JAMILA’S MEMO: A letter to President William Ruto
Audio By Vocalize
Hujambo Mheshimiwa Rais William Ruto. Ni siku
mbili sasa tangu uapishwe rasmi kama rais wa tano wa Jamhuri ya Kenya. Hafla ya
kuapishwa kwako ilikuwa na mbwembwe na sherehe, lakini pia ilikuwa na matumaini
makubwa miongoni mwa Wakenya wengi; matumaini kuwa maisha yao yatakuwa bora
zaidi, matumaini kwamba ahadi ulizotoa za kuimarisha maisha ya mwananchi na
kumpunguzia changamoto za kila siku zitatimia.
Tayari umewaapisha majaji sita wa mahakama,
na kutimiza mojawapo ya ahadi ulizotoa, na kuwapa wananchi matumaini ya kupata
haki wanapoelekea mahakamani. Kuimarisha huduma za idara ya polisi kwa kuweka
mikononi mwa inspekta jenerali wa polisi mkoba wa kuendesha shughuli za idara
hiyo; matumaini kuwa wananchi waatakapokimbia kwa polisi kutafuta usaidizi,
wataupata kwa haraka.
Bei ya mbolea, na pembejeo za kilimo ambazo
wakulima wanaweza kumudu, itakuwa afueni kwa wakulima na Wakenya wote kwa
ujumla. Gharama ya maisha iko juu, wengi wanashindwa hata kupata chakula cha
kulisha familia zao; utakuwa umewaondolea mzigo mkubwa iwapo bei ya chakula
itakuwa nafuu.
Masomo kwa watoto na uwezo wa wazazi
kugharamia masomo hayo ni jambo linguine. Hali ngumu inawakumba wazazi wengi
ambao wanahangaika kila mara shule zinapofungwa kwani tayari wanafikiria karo
itatoka wapi shule zitakapofunguliwa, na ahadi za elimu bora kuliko bora elimu,
miundo mbinu shuleni, walimu wa kutosha, nafasi shuleni na mtaala unaofaa.
Ahadi za ajira kwa vijana na nafasi zaidi
kwao kuendelea mbele katika maisha yao; wengi wanahangaika usiku na mchana
wakitafuta nafasi yoyote, popote pale angalau wapate cha kuweka mfukoni. Na sio
kwa sababu hawajasoma, la, wengi wao wamehitimu ila stakabadhi hizo sasa
zimekuwa mzigo wa kubebwa hapa na pale kutafuta nafasi za kazi. Vijana hawa
wanakutazama wakisubiri kutimizwa kwa ahadi yao.
Wanaoendesha biashara ndogo ndogo na
wanaohitaji kupewa usaidizi kuanzisha biashara pia wako hapo pembeni. Iwapo
watu wengi zaidi watapata mazingira bora ya biashara na usaidizi wa kuanza na
kuendelea na biashara zao, idadi ya wale wanaosubiri kuajiriwa itapungua; wataweza
kujitegemea na kusaidia familia zao.
Na kwa wanawake je? Wanasubiri nafasi
uongozini, ni furaha kubwa kushuhudia kina mama zaidi wakichaguliwa na wananchi
katika nyadhifa za juu; ishara tosha kwamba wananchi wanaanza kuwa na imani na
uongozi wa mama. Na bado wanawake wanasubiri ahadi kwao ya nafasi zaidi
serikalini. Itakumbukwa kuwa Rais Ruto aliahidi kuwa asilimia 50 ya baraza la
mawaziri litakuwa ni wanawake; mbali na hayo, juhudi za kuwasaidia kupata
mazingira bora ya kufanya biashara zinasubiriwa.
Huduma bora hospitalini; kuwepo kwa
madaktari, wauguzi, dawa na vifaa vya kutambua magonjwa. Wengi wanatarajia
wataweza kumudu gharama inayoambatana na matibabu, wamechoshwa kuwatazama
wapendwa wao wakihangaika kwa kukosa huduma bora za matibabu.
Unaona mheshimiwa rais, mahitaji ya wananchi
sio mengi; chakula cha kila siku, masomo kwa watoto, nafasi za ajira, huduma
bora za matibabu ni mambo muhimu kwa mwananchi wa kawaida. Safari yako ndio
inaanza, sio safari rahisi, macho ya mamilioni ya Wakenya yanaelekezwa kwako na
serikali utakayounda. Na bila shaka kutakuwa na panda shuka za hapa na pale, ila
ukiweka kipaumbele mahitaji ya wananchi na kutimiza ahadi za kuimarisha maisha
yao, utakuwa umefaulu machoni mwao.
Na mwisho kabisa Rais Ruto, huu ni wakati wa
kumfikiria kila Mkenya, yule aliyekupigia kura na yule ambaye aliweka kura yake
kwingine. Itakuwa bora ukiweka juhudi zaidi kuwapa mkono Wakenya ambao huenda
wanaona hawamo ama hawana nafasi popote kwa sababu kiongozi wao alishindwa. Na
kwamba sio wote waliokuwa nawe wakati wa kampeini watakufaa serikalini, unakumbuka
rais mstaafu Moi alisema uongozi ni tofauti.
And that is my Memo!

Join the Discussion
Share your perspective with the Citizen Digital community.
No comments yet
This discussion is waiting for your voice. Be the first to share your thoughts!